
USIKU WA JAN. 20, 2005
***** ***** ****** *****
ILITOKEA kupenda kupiga gitaa tangu nikiwa na umri wa miaka 14. Lakini nilipenda kupiga baada ya kaka yangu ambaye katika familia yetu alitokea kuwa naye karibu takriban kwa kila jambo. Aliitwa Barack Ambrosse Ndayanse.
Barack alikuwa mpenzi zaidi wa gitaa na alikuwa akipiga na rafikiye kipenzi Ramadhani Zahoro, wakitoroka darasani na kwenda kujificha kwenye shamba la mihogo na kuanza kupiga gitaa lililotengenezwa kwa zana hafifu za galoni la lita tano za maji.
Kwa kuwa mara kwa mara nilikuwa nashinda naye, nilishawishika na mimi kujifunza kutekenya nyuzi za gitaa hilo la kienyeji.
Mieze kadhaa baadaye tukajikuta kwenye kwaya ya Kanisa la Anglikana Mwanga mjini Kigoma na wakati huo walikuja wanamuziki wawili kutoka katika kwaya iliyokuwa ikitikisa ukanda wa Afrika Mashariki, Mwanza Town Choir.
Wanamuziki hao walikuwa wamekuja mjini Kigoma kwa ajira za Upanuzi wa Bandari na hivyo wakaamua kuwa wanakuja kanisani hapo kupiga magitaa.
Ni hapo ndipo mimi na Barack tulipogundua kuwa viwango vyetu vilikuwa duni sana na kuanza kujifunza kwa hao vijana waliotoka Mwanza.
Tuliendelea na fani hiyo na mimi nikajikuta nikikomaa zaidi katika gitaa la solo kiasi cha kujikuta nikianza kupiga katika bendi moja iliyokuwa mjini hapo ya Super Kibisa Orchestra tukiwa na Ramadhani Zahoro ‘Bangwe’ ambaye kwa sasa ni mpigaji gitaa tegemeo wa Msondo Ngoma Music Band.
Hata hivyo, baadaye Ramadhani aliondoka Kigoma na kulivaa jiji la Dar es Salaam, mimi na Barack na wanamuziki wengine tukabaki tukiliendeleza ‘sebene’ kwenye bendi hiyo na wakati huohuo pia tukiupiga muziki kwenye kwaya.
Hiyo ni ile miaka ya 1980-1989.
Kuanzia mwaka 1990, kasi ya kupiga muziki ikanipungukia na hiyo ni kwa sababu nilibaini kuwa sikuwa napenda sana fani hiyo bali tu ni kwa ajili ya kuhimizwa na ndugu yangu. Sasa nikahamia jijini Dar es Salaam na nikawa napiga gitaa mara chache pale nilipoliona.
Siku zikaenda hatimaye nikajiunga na Kwaya ya KKKT Hananasif Kinondoni, kwa maombi ya mwalimu mmoja aliyewahi kuniona nikipiga gitaa mahali fulani. Hapa Hananasif nimekaa sana na kwa kuwa ndipo yalipokuwa masikani yangu nikajikuta nikirudi kwenye fani kwa kasi ya ajabu.
Mapenzi yangu kwa mpiga solo mahiri wa enzi za miaka ya 90, Alain Makaba wa Wenge BCBG yakairudisha ile ari yangu ya kupiga gitaa na hasa kwa kipindi kile Wenge walipoibua albamu ya Pentagone mwaka 1994.
Sasa nikarudi kwenye gitaa kwa nguvu kubwa. Kila wimbo uliopigwa na Alain Makaba nikawa nauiga na kwa kiasi kikubwa. Kiwango kikapanda. Mwishoni mwa miaka ya 1990, African Stars ‘Twanga Pepeta’ wakazaliwa. Nakumbuka bendi hiyo ilikuwa inapiga muziki wake kwenye viwanja wa Leaders Club bureee! Kila Jumapili mchana!
Watu tukawa tunajimwaga hapo kila wikiendi na hasa kwa kuzingatia kwangu mimi pale palikuwa ni jirani sana na nyumbani.
Mpangilio mzuri wa muziki wa Twanga sanjari na upigaji wa Adolf Mbinga katika gitaa la solo vilinivuta sana na hivyo sasa nikawa nikibuni vyangu, nachanganya na vionjo vya ama gwiji Alain Makaba au mzalendo Adolf Mbinga hasa na wimbo wake wa Kisa Cha Mpemba.
Nikaendelea kuwa bora katika fani hiyo huku pia nikifanya kazi ya ajira katika Kampuni ya Uchapishaji ya Heko.
JANUARI 20
Hii ilikuwa ni siku, kama siku nyingine ambazo niliamka na kwenda kwenye shughuli zangu za kila siku. Ilipofika jioni, kitu kama saa 11 hivi nikawa nimesharudi Kinondoni na moja kwa moja nikaelekea kanisani kwa ajili ya mazoezi ya kwaya. Mazoezi yalimalizika saa 1 usiku. Kijigiza kilikuwa kimekwishaitawala anga.
Baada ya mazoezi nilitoka na rafiki yangu, Zawadiel Kimambo aliyekuwa akiishi Kinondoni Shamba. Nilikuwa nikimsindikiza na tulikuwa na mazoea ya kuzungumza kuhusu hili na lile hususan kuhusu kwaya kila tumalizapo mazoezi.
Siku hiyo, mara tulipomaliza mazoezi nilichoropoka hadi nyumbani ambako hakukuwa mbali. Nikavua viatu na kuvaa kandambili kwa kuwa siku hiyo sikuwa natarajia kwenda mbali. Nikarudi eneo la kanisa ambako nilimkuta Kimambo akiwa nje ya uzio akizungumza na wanakwaya wengine huku akinisubiri.
Mara tu nilipofika Zawadiel alisitisha maongezi na kuniambia, “Inno twen’zetu.”
Tukaondoka taratibu. Tukapita jirani na shule ya Msingi Hananasif katika eneo lilikokuwa na miti mingi iliyoongeza nguvu ya giza kwa kuwa hakukuwa na nyumba zilizokuwa kando ya barabara.
Tukawa tunashika Mtaa wa Ngano, mtaa uliokuwa umepandwa miti mingi iliyounda kivuli kizito mchana na kutengeneza giza la kuogofya usiku.
Mazingira yale tulikwishayazoea hivyo hatukuwa na wasiwasi wowote. Tukawa tukitembea taratibu huku tukizungumza.
Hatimaye tuliuacha Mtaa wa Ngano tukashika Mtaa wa Wakulima. Mbele kidogo tukawa tunapita katikati ya makaburi. Tulipofika mwisho wa eneo la makaburi, tukawa kando ya Barabara ya Kinondoni, eneo lililojulikana na linalojulikana mpaka sasa kwa jina la MWEMBEJINI.
Hapo tulikuta mchanganyiko wa watu. Walikuwepo waliokuwa kituoni wakisubiri daladala na wengine kwa harakaharaka unaweza kuwaita ‘vibaka’ au ‘mateja kwani walikuwa ni vijana wanne wakizunguka-zunguka tu kituoni hapo huku wakizungumza kwa sauti zenye mikwaruzo inayokera, sigara na bangi zikivutwa bila ya wasiwasi.
Mimi na Zawadiel hatukuwajali kama ambavyo nao hawakutujali. Mara kwa mara watu wa aina ile huwa eneo lile wakivizia daladala ili waingie na kubanana na abiria na matokeo yake abiria ‘hulizwa.’ Au huvizia abiria atakayeteremka na kuzubaa-zubaa na wao huwa wepesi kwa kumpora chochote chenye manufaa kwao.
Tulivuka barabara na kuendelea na safari, nikiendelea kumsindikiza rafiki yangu kipenzi, Zawadiel.
“Tuingie pale kwenye kantini tunywe maziwa moto,” Zawadiel aliniambia mara tulipokuwa upande wa pili wa barabara.
Sikuwa na sababu ya kukataa. Nikamjibu, “Poa tu.”
Tukaingia. Akaagiza maziwa moto na keki mbili. Tukanywa taratibu huku tukiendelea kuzungumzia mambo ya muziki wa gitaa, fani iliyokuwa inayateka maongezi yetu kila tunapokuwa pamoja.
Nusu saa baadaye, kama saa 2 hivi, tuliagana, yeye akaendelea kwenda kwake ambako kwa hapo hakuwa mbali sana na mimi nikaanza safari ya kurejea nyumbani Hananasif. Kumbuka nilikuwa nimetoka nyumbani na kandambili tu miguuni na sikutarajia kuwa ningetembea mpaka huko Kinondoni Shamba.
Hata hivyo, nilijifariji kuwa kwa giza lililokuwapo isingekuwa rahisi kila mtu kubaini kuwa nimevaa nini miguuni. Sikujali. Nikaanza kuvuta hatua, nikavuka barabara huku nikiwa nimekifungua kijiredio changu kidogoooo aina ya Panasonic nikisikiliza muziki.
Wakati niko eneo la katikati ya makaburi, nikimulikwa na mwangaza mkali kutoka kwenye taa kubwa zilizolizingira jengo moja lenye ofisi nyeti sana serikalini, mara nikakutana mwanamama mmoja mnene kiasi akiwa amejitanda kanga kutoka kichwani.
Dada huyo akanichangamkia haraka, “Kaka, mambo?”
“Poa tu,” nilimjibu na kumtazama kidogo kisha nikaendelea na safari yangu. Hakuniachia. “Anko samahani kidogo,” aliniambia huku akiwa amesimama na kunigeukia.
Nikaiheshimu kauli yake. Nikasimama na kumsikiliza.
Akanisogelea. Tukawa jirani sana. Tukatazamana. Nikahisi manukato makali kutoka maungoni mwake huku tabasamu likichanua usoni pake na jino moja sijui la dhahabu au mfano wa dhahabu likajitokeza kinywani mwake.
“Vipi?” hatimaye alisema kwa mnong’ono wa kibiashara zaidi huku akinishika mkono.
Kwa kuwa nilikuwa mwenyeji wa eneo hilo sikuhitaji kujiuliza ni kpi kilichomfanya mwanadada huyu anisimamishe. Watu wa aina yake muda huo huwa wameshatanda kando ya Barabara ya Kinondoni pale Mwembejini, kule kwenye makaburi ya ‘Lang’ata’, kwenye njiapanda ya kuelekea Leaders Club pale Tunisia Road hadi maeneo mengine ya huko Ada Estate wakiwa mawindoni, wakivizia mwanamume ‘mwenye njaa.’
Sikutaka kumjibu vibaya aliyenigeuza mimi kuwa windo lake. “Poa tu,” nami nilimjibu kwa sauti ya chini, nikimruhusu aendelee kukishika kiganja cha mkono wangu na wakati mwingine kukitomasa-tomasa.
“Inakuwaje?” akarusha swali na kumalizia, “twen’zetu basi tuka…” alichomalizia kukitamka kilikaribia kunichekesha kwa kuwa nilitarajia ndivyo angesema.
Hata hivyo sikucheka. Nikaendelea kuonesha kumjali. Nikamjibu kwa upole, “Usijali, tufanye siku nyingine. Leo siko fresh,” nikaongeza huku nikijipapasa mifuko kuonyesha kuwa sikuwa na pesa.
“Una ngapi sh’ngapi?” aliniganda.
“Sina kitu,” kwa kiasi fulani nilianza kuchukia. Hawa viumbe wenye biashara hizi mara nyingi huwa ving’ang’anizi! Na ukiwachekea utajuta!
Akanitazama usoni na kugundua kuwa sasa sikuhitaji kuendelea kujadili kuhusu hiyo hoja yake na wala sikuwa nahitaji kuwa naye. Akaniachia mkono huku kwa unyonge akisema, “Poa, acha sie tukapuyange viwanja…”
Sikumjibu.
Nikaendelea kuvuta hatua taratibu hadi nilipofika kwenye Mtaa wa Ngano. Kama awali mtaa huu ulikuwa umetulia lakini sasa niliona kama ukimya ulizidi. Mara ghafla nikasikia upepo mkali ukivuma, upepo ulioambatana na kimbunga kidogo. Vumbi likatimka mbele yangu, hatua kama kumi hivi. Miti ikatikisika kwa nguvu!
Nikashangaa kisha nikajawa na hofu! Haukuwa upepo wa kawaida!
Mara mbele kidogo, kushoto ambako kulikuwa na kijibaa kidogo chenye wateja wachache kukazuka kelele kali kwa sauti kama ya mwanamke. Punde msichana aliyevaa blauzi pana na suruali akatoka mbio akikimbilia barabarani akija huku nilikokuwa!
Aliponifikia, akanitazama kidogo kisha akanipita na kuendelea kukimbia akielekea Mwembejini. Sikumjali. Nikaendelea kutulia palepale nikiangalia eneo lile la mbele yangu ambako upepo uliokuwa ukivuma sasa ulianza kupungua taratibu.
Hatimaye hali ikatulia, nami nikaanza kutembea tena. Nikavuta hatatua taratibu huku nikihisi kutokuwa na utulivu moyoni.
Nilipofika jirani na kile kijibaa, upepo ukaanza kuvuma tena! Kwa msaada wa mwangaza mdogo wa taa zilizokuwa zikiwaka ndani ya baa hiyo nikafanikiwa kuona kitu kama kamba ndefu mbele yangu. Kamba nyeusi. Nilijenga imani kuwa ni kamba kwa kuwa kitu hicho kilikuwa kimetulia tuli kandokando ya barabara.
Sikuwa na wazo lolote toafuti kuhusu kitu hicho, nikaendelea kutembea hadi nikawa hatua kama mbili hivi kutoka mbele ya kitu hicho.
Haikuwa kamba!
Alikuwa ni nyoka! Na hakuchelewa, alijivuta kwa kasi na kutua kwenye kiganja cha mguu wangu wa kulia, akadonoa haraka kisha kwa kasi ileile akajivuta na kuingia nyasini, kando ya barabara!
Eneo aliloingia kiumbe huyo hatari kulikuwa na ua kubwa lililotengeneza chaka la aina yake hivyo niliishia kusikia sauti ya, “Shhhhh…ssshhhhh….” ishara ya kutokomea ndani ya chaka hilo lililokuwa jirani sana na kijibaa hicho.
Lilikuwa ni tukio la haraka sana na hata maumivu yake pia yalikuja kwa kasi vilevile! Dakika ya kwanza niliweza kukanyaga chini mguu. Nilipovuta hatua moja, nilipokanyaga tena chini maumivu nliyoyasikia hayakuwa ya kawaida! Yalikuwa makali kuliko unavyoweza kukadiria.
Nikahisi uhai unakaribia kunitoka! Jasho likaanza kunitoka! Sikuona mtu yeyote mbele wala nyuma! Maumivu yakazidi! Nikalazimika kuushika mguu ulidungwa jino na joka lile, nikaukunja juu-juu kwa nyuma na kusimamia mguu wa kushoto pekee japo kwa shida.
Nilipozidiwa nikajikuta nikianguka chini, katikati ya barabara huku kwa mbali nikisikia sauti ya mtu akicheka, Sauti ya kike!
NILIANZA kukata tamaa ya kuishi. Simulizi nyingi nilizokwishazisikia tangu utoto kuhusu madhara ya kuumwa na nyoka ziliniletea kumbukumbu ya kuogofya akilini mwangu. Nikatulia chini, katikati ya barabara huku nikiangalia huku na kule na kuomba Mungu atokee mtu wa kunisaidia.
Hatimaye haikutimu hata dakika moja, mtu mmoja, mwanamume akatokea ndani ya kile kijibaa, akitembea kwa kasi lakini akionekana kutokuwa na wasiwasi wowote. Huenda alikuwa akiwahi nyumbani kwake. Aliponiona, akashtuka na kunisogelea.
“Vipi?” ndivyo alivyoniingia.
“Nyoka!” nlimjibu. Sasa maumivu yalikuwa yakizidi na kwa hali hiyo nikawa najikunja na kujikunjua pale chini huku nimeushika mguu uliojeruhiwa.
“Hee!” alibwata kwa mshtuko.”Atakuwa ni yule nyoka tu….duh!”
Akanishika mkono na kunisaidia kunyanyuka. “Jitahidi kujikokota tufike hata pale kwenye ile nyumba.”
Mbele yetu kulikuwa na nyumba ambayo nilisikia kuwa ilikuwa inamilikiwa na Meya wa moja ya manispaa za Jiji la Dar.
Nilitembea kwa mguu mmoja wa kushoto huku wa kulia nimeukunja juu kwa nyuma na jamaa yule kapenyeza mkono wake kwapani kwangu kulia ili kuwa mhimili mzuri wa kutembea.
Nikawa narukaruka hadi kwenye hiyo nyumba ambayo ilikuwa hatua kama kumi na tano au ishirini hivi kutoka pale nilipokumbwa na zahama.
Tulipofika kwenye nyumba ile tukapokewa na binti mmoja na kijana mmoja wa kiume wanaosadikiwa kuwa walikuwa wakiilinda tu nyumba hiyo. Taarifa za kuumwa kwangu nyoka zikazidi kuenea tangu nilipofika hapo. Dakika tano baadaye watu saba walikuwa ndani ya nyumba hiyo, mmoja wao akiwa ni mzungu wa asili ya Uholanzi, ambaye alikuwa akiishi jirani na nyumba hiyo akiwa pia na ofisi ya shirika lake binafsi hapohapo.
Yule mzungu ndiye aliyeonekana kutaharuki zaidi alipoisikia taarifa yangu. Akawa akihaha huku na kule kusaka kamba ya kunifunga mguuni ili sumu isisambae. Vijana wengine waliokuwa pale nao walikuwa wakihangaika kivyao, baadhi yao wakionekana kuogopa kuwa labda nyoka huyo atazuka tena na kumdhuru yeyote kati yao. Baada ya dakika kadhaa mmoja akaja na waya wa umeme na wembe.
“Mchanje kwanza!” mmojawao alisema.
Nikachanjwa juu kidogo ya kiganja cha mguu! Damu nzito kama tope, damu nyeusi tii ikatoka kama mabonge fulani hivi. Wote walioshuhudia wakashtuka! Mimi nikaogopa!
“Chanja tena juu yake!”
Ushauri ukatolewa na mwingine.
Mwenye wembe akachanja mara mbili umbali kama wa inchi tatu, juu ya pale alipochanja awali.
“Heee…” wakazidi kubwata kwa mshangao. Hata hapo ilitoka damu nzito na nyeusi kama tope.
Wakachanja sehemu kama nne tofauti mpaka jirani sana goti na pote pakaonyesha kuwa tayari pameathiriwa na sumu ya joka lile.
Mguu ukatapakaa damu! Haukupendeza kutazamwa! Mabonge bonge hayo ya damu yakawa yakishuka taratibu na kunitisha hata mimi mwenyewe!
Kilichonitia woga ni kuwaona hata hawa vijana waliokuja kunisaidia nao wakionekana kutaharuki. Baadhi walikuwa wakinikodolea macho tu bila ya kufanya chochote.
Hatimaye yule aliyekuwa akinichanja mguuni akasema, “Kunja suruali zaidi bro!”
Nikafanya alivyotaka. Nilikunja suruali hadi mapajani.
Akachanja kwenye paja mara tatu. Damu iliyotoka hapo ni ile ambayo wenyewe tumeizoea kuwa ni damu ya mwanadamu yeyote. Haraka jamaa huyo akaamua kuitumia kamba ya katani iliyokuwa imeletwa hapo na kijana mmoja wa Kiarabu ambaye alitoka kwenye nyumba kama ya tano hivi baada ya kusikia kuhusu tukio hilo.
Nikafungwa kamba hiyo kama vile ni mtu ninayezuiwa kutoroka. Ilikazwa kisawasawa kwenye paja ikiaminika kuwa itasaidia kuizuia sumu kupanda zaidi na kuleta madhara zaidi.
Kilichofuata ni kukabidhiwa fimbo ya kunisaidia kutembea mpaka nje, kando ya barabara ambako yule kijana wa Kiarabu alikuwa kaegesha gari dogo aina ya Toyota Mark 11 na nikaingia ili wanipeleke hospitali.
“Usihofu tena,” yule kijana wa Kiarabu ambaye nilikuwa nimeketi naye katika kiti cha nyuma aliniambia. Kisha akavuta suruali juu na kunionyesha mguu wake wa kushoto ulivyobabuka! Ulikuwa unatoka magamba kuanzia chini mpaka kwenye goti!
“Unaona hii?!” aliniuliza huku akinitazama usoni kwa macho makali.
Sikumjibu, nikautazama tu ule mguu, tendo nililoamini kuwa lilitosha kumfanya ajue kuwa nimemsikia.
“Joka hilo!” alisema. “Nina wiki kama tatu hivi tangu liniume. Nilikuwa nimekaa hapo nyumbani, nje nikipunga hewa. Likatokea huko lilikotoka, kasi ile mbaya, liliponifikia tu likaning’ata na kuteleza msh’kaji wangu. Jeusi na refu kishenzi! Nilipiga kelele mshkaji wangu, akaja faza na kijiwe f’lani hivi sijui kakitoa wapi… akaniwekea mguuni, nasikia huwa kinafyonza sumu.
“Halafu wakanipeleka Agakhan Hospital. Ningekufa! Yaani ni kama niliponea chupuchupu! Wiki nzima sikuweza kutembea. Sasa nimepona lakini cheki nimekuwa kama nyoka au kenge kudadek! Magamba haya nd’o yanatoka…sijui nd’o ngozi iliyoharibiwa na sumu?!”
Nilimwelewa lakini sikumjibu kitu. Mawazo yangu yalikuwa juu ya zahama iliyonikuta. Nikamkumbuka mke wangu. Nikawaza, je, atawaza kuwa niko wapi? Anaweza kuwa na mawazo dhaifu akafikiria kuwa nimekwenda kwa mwanamke wa pembeni? Nimpigie simu?
Swali hili la mwisho nikaona ndilo linapaswa kufanyiwa kazi. Hata hivyo, usalama kwanza! Ndivyo nilivyoamini. Nikatulia huku nikiyasikilizia maumivu ya jeraha na zile chale ambazo nazo ziliongeza maumivu huku nikizidi kutishika kila nilipoutazama mguu huu na kushuhudia damu hiyo yenye mabonge-bonge mazito ikizidi kutoka kwenye yale maeneo yenye chanjo za wembe.
Gari likaenda hadi eneo la Mkwajuni ambako tuliingia katika zahanati moja ya MICO. Daktari akatupokea kwa moyo mkunjufu na kuniangalia kwa macho ya huruma. Baada ya kupata maelezo akasema, “Ni tatizo kubwa kwa upande wetu hapa kwenye zahanati. Sisi hatuna uwezo wa kukuhudumia lakini kwa kupunguza tatizo ili sumu isiende kudhuru figo, nitakuchoma sindano moja ya kinga halafu itabidi uende Mwananyamala.”
Wale wasamaria walionileta waliposikia hivyo wakamshukuru daktari na kuniambia kuwa wao wanarudi nyumbani kwa kuwa hata gari lao halina mafuta ya kuweza kunipeleka huko Mwananyamala.
Nikajua kazi ninayo. Hata hivyo, nikawashukuru kwa msaada huo wa kunifikisha hapo. Nikajali kwanza kupata huduma hiyo ya sindano. Na nilipokwishachomwa, nikatoka nje na fimbo yangu dhaifu huku bado damu ikizidi kunitoka kwa wingi na baadhi ya watu wakawa wakiniangalia kwa mshangao bila ya msaada.
Nikaanza kujikokota nikielekea kituo cha daladala huku nikiwaza je, kuna daladala itakayonikubali kwa hali ile niliyokuwa nayo? Guu limeshavimba na limetapakaa damu nyeusi ti! Nikajisikia kukata tena tamaa!
Nikajikokota tu bila ya matumaini hatua kama kumi hivi, jamaa mmoja akanisimamisha na kuniuliza, “Vipi aisee?”
Nikamtazama na kugundua kuwa ni fundi makenika ambaye tulikuwa tukikutana mara kwa mara jirani na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Usharika wa Azania katikati ya jiji akitengeneza magari katika kijigereji bubu kilichokuwa katika eneo hilo. Jamaa huyo ambaye siwezi kulisahau jina lake, Lyimo, alikuwa msaada mkubwa kwangu kwa siku hiyo.
Japo tulifahamiana, lakini hatukuwa na ukaribu, ni kule kujuana-juana tu kimjini-mjini kama ilivyo kwa wakazi wengi wa Jiji la Dar. Lakini usiku huu wa saa tatu kasoro jamaa huyu alisitisha kuendelea na safari pale tu nilipomdokeza mkasa ulionikuta.
Hatua chache kutoka pale tulipkuwa kulikuwa na teksi mbili zimeegeshwa. Haraka akamwita teksi dereva mmoja na kumwambia, “Danny, mpeleke mshkaji wangu Mwananyamala hospital haraka.”
Dereva yule aliniangalia kwa mshangao na kuniuliza, “Umekumbwa na mkasa gani?”
“Huu siyo muda wa maswali!” Lyimo aliingilia kati. “Mpeleke halafu ukirudi uje kuchukua pesa yako.”
Dereva alinifungulia mlango wa kushoto, mbele huku akiniambia, “Ingia msh’kaji.”
Kisha Lyimo akaniuliza, “Nyumbani wana taarifa?”
Ni hapo nilipojiwa na kumbukumbu kuhusu umuhimu wa kufikisha taarifa nyumbani. Nikamjibu kuwa hakuna taarifa na nikampa namba mbili za simu, moja ya rafiki yangu na nyingine ya mke wangu.
“Simu yangu haina salio na inaweza kuzima muda wowote,” nilimwambia. “Tafadhali, ukiweza nisaidie kuwapigia kuwapa taarifa.”
“Usijali nitahakikisha taarifa inafika. Nikishindwa basi nitapita hata pale kanisani na kuwataarifu.”
Teksi iliondoka na kwa kweli yule dereva alikuwa na moyo wa kibinadamu zaidi kwani tulipofika Hospitali ya Mwananyamala hakuniachia getini. Alinishika mkono na kunipeleka hadi kwa daktari huku wagonjwa wengine wakituruhusu kuwapita kwa kuwa hali yangu iliwatisha na kuonekana kuwa napaswa kupewa kipaumbele katika huduma.
Baada ya kutoa maelezo kwa dakatri, nikakalishwa kwenye kiti maalum na dereva huyohuyo wa teksi, akanisaidia kwa kukisukuma kiti hicho hadi wodi namba 5 ambako nilikabidhiwa kitanda. Usiku huo wa Alhamisi ukanikuta hapo hospitali na ukaisha nikiwa hapo hospitali.
Siku iliyofuata ilikuwa ni Sikukuu ya Maulid. Siku ya mapumziko. Mimi nilikuwa wodini. Ndugu, jamaa na rafiki walifika hospitali kuniona. Wanakwaya wengi pia walifika kuniona. Lakini hadi kufika jioni sikuwa nimepata huduma yoyote kubwa kuhusu jeraha hilo zaidi ya kupewa tembe za kutuliza maumivu! Mguu ulizidi kuwa mweusi hususan eneo la kiganjani. Na uvimbe ulizidi!
Kila nilipojaribu kuhoji kwa nesi kuhusu kuhudumiwa nilipata majibu yasiyoelewaka. Mara, “Dokta atapita…” mara “vuta subira madokta wako kwenye kikao…” mara hili mara lile ilimradi yalikuwa ni majibu yasiyokuwa na msaada wowote kwangu.
Hatimaye usiku ukaingia bila ya kupata huduma yoyote! Ilipofika saa 4 nesi mmoja akaniletea vidonge vya vallium ili nipate usingizi. Nikanywa na vikanisaidia kwa kiasi fulani.
Asubuhi ya siku ya Jumamosi mambo yakawa vilevile. Hadi saa 4 bado sikuwa nimemwona daktari yeyote aliyefika kunihudumia. Kungekuwa na mgomo rasmi uliotangazwa na madaktari labda ningeelewa lakini hakukuwa na mgomo wa wazi labda wa siri.
Hatimaye saa 7 mchana ikatinga, bado sijaona mtu. Nilipoletewa chakula kutoka nyumbani nikala kama kawaida kwani jeraha lile halikunifanya nishindwe kula. Lakini nilishangazwa na huduma za hospitalini hapo. IIipotimu saa sita hivi nikamwona mwanamume mmoja amevaa joho jeupe la kidaktari akipita kitanda kimoja hadi kingine. Hatimaye akafika kwangu na kukiangalia cheti kwa muda kisha akaandika-andika maandishi aliyoyajua mwenyewe kisha akawa ananiangalia mguu hatimaye akaondoka. Sikumwona tena kwa siku hiyo na wala sikumwona muuguzi yeyote mwingine.
Usiku saa 4 nikapewa tena vallium ili nisinzie!
Nikasinzia.
Asubuhi ya siku ya Jumapili nikawa nimekwishakata tamaa ya kuhudumiwa katika hospitali hiyo kubwa zaidi ya serikali wilayani Kinondoni.
Wakati kaka yangu Barack (sasa ni marehemu) alipokuja akifuatana na rafiki yangu mkubwa, askari wa JWTZ, Mathew Mapunda SAA 7 mchana, tayari nilikuwa nimekuwa na uamuzi wa kuondoka hospitalini hapo. Na wao walipofika walikuwa na wazo kama langu. Hata hivyo, kabla ya kuchukua uamuzi, tulimuuliza nesi mmoja aliyekuwa akirandaranda humo wodini, nesi ambaye kwa kiasi fulani nilikuwa nimekwishazoeana naye.
“Ni kwa nini sijahudumiwa mpaka leo?”
Nesi yule alitabasamu kidogo kisha akaniambia kwa sauti ya chini, “Kaka si kwamba madaktari hawapo …wapo sana..wamejaa tele ka’ pishi ya mchele. Wanajichimbia kule theatre (chumba cha upasuaji) wakingoja dili. Kama una pesa leta nikamwone daktari aje akuhudumie. Vinginevyo kaka’angu…mmmh” akaiacha sentensi hiyo ikielea.
Nilimwelewa.
Kaka yangu na rafiki yangu walikuwa na pesa lakini kwa hasira yule rafiki yangu alisema, “Hapa hapafai! Hakuna kutoa pesa wala nini…tuondoke zetu!” akamgeukia yule nesi na kumwambia kwa ukali, “Tunaondoka na mgeni wetu!”
“Hatukatai lakini subirini basi tufanye utaratibu wa ‘kumdischaji’.”
“Nini?! Hatuna muda mchafu!” kaka yangu alifoka huku akipunga mkono hewani. “Hatusubiri chochote! Tunaondoka naye!”
Mathew na kaka yangu wakatoka, wakielekea nje ya geti. Wakati huo wanakwaya takriban kumi na watano nao walikuwa nje ya wodi wakiwa wamekuja kunijulia hali na kujua hatima ya sakata lililonikabili.
Dakika chache baadaye kaka yangu na Mathew wakarejea wakiwa ndani ya gari pick-up, nikapanda na wanakwaya wengine wakapanda tukasepa!
Moja kwa moja hadi Kinondoni Mtaa wa Sekenke ambako kulikuwa na zahanati iliyokuwa ikisifiwa kipindi hicho; Nyamongo. Ile kufika tu nikapewa tembe moja ndogo kisha nikachomwa sindano moja. Nikapewa kitanda ndani ya chumba nikiwa peke yangu!
Nikalazwa kwa mara ya pili!
Nikatundikiwa dripu tatu mfululizo! Jumatatu asubuhi, Januari 24 nilikuwa na nafuu kubwa. Japo maumivu ya mguu bado yalikuwapo lakini hayakuwa ya kutisha! Na ilipofika jioni niliruhusiwa kuondoka.
SIKU MBILI BAADAYE
Wakati nikiwa nyumbani nikiuguza jeraha walikuja watu kadhaa kunijulia hali. Baadhi yao ndio waliozungumza kuhusu tukio la nyoka yule na imani za kishirikina. Kuna waliodai kuwa joka lile lilikuwa likifugwa na mama mmoja wa Kiarabu aliyekuwa akiishi jirani sana nyumba ya Shule ya Msingi Hananasif, na kwamba mama huyo alikuwa amechoka kuendelea kumfuga hivyo akamwachia.
Ikadaiwa kuwa nyoka huyo amekwishawauma watu wanne, mimi nikiwa mmojawao kwa kipindi cha wiki mbili!
Na ikaendelea kudaiwa kuwa mara kwa mara kila ifikapo usiku pale kwenye makutano ya Barabara za Wakulima na Ngano, jirani kile kijibaa, husikika kelele za kicheko cha mwanamke asiyeonekana!
Siku ya tatu gazeti maarufu kwa siku zile, ALASIRI lililokuwa likichapwa na kampuni ya The Guardian Ltd, likachapa kwa kirefu habari yeny kichwa cha: JOKA LA MAAJABU LAITIKISA HANANASIF. Habari hiyo ikawafanya wakazi wengi wa eneo hili wagwaye kupita Barabara ya Ngano iwe asubuhi mchana hata jioni au usiku.
Ni wengi walioogopa siyo wote. Baadhi walipita lakini wakiwa na hadhari kubwa na kikafika kipindi kila mtu alikuwa akipita mtaani hapo macho yake yanakuwa juu ya miti akihofia kuwa huenda joka hilo liko mtini na linaweza kumshukia mtu yeyote.
Siku mbili baada ya gazeti hilo kutoa habari hiyo, dada mmoja (sasa ni marehemu) aling’atwa na nyoka njiapanda ya barabara hizo za Wakulima na Ngano zikiwa ni kama hatua hamsini tu kutoka pale nilipong’atwa mimi.
Huyo hakuwa peke yake, alikuwa na mdogo wake ambaye alihadithia simulizi isiyotofautiana na madhila yaliyonikuta mimi ile Januari 20. Kwamba, muda mfupi baada ya dada yake kuumwa na nyoka, kicheko kikali kikasikika kutoka kwenye mkusanyiko wa miti uliounda chaka zito kwenye makutano hayo.
Kisha kukazuka upepo mkali kwa muda mfupi na kutoweka. Lakini tofauti ndogo ni kuwa siku hiyo hakukuwa na mtu aliyezuka mbio na kuwapita pale kama ile siku yangu na yule mwanamke.
Hata hivyo, dada yule ambaye alikuwa akiishi hukohuko Hananasif alikata roho muda mfupi baada ya kufikishwa hospitali huku mwili wote ukiwa umebadilika rangi na kuwa mweusi ti!
Wiki moja baada ya dada huyo kufariki nikapata taarifa kuwa hata yule kijana wa Kiarabu ambaye alinipa msaada wa kunipeleka Hospitali ya MICO pale Mkwajuni kwa huduma ya awali, akiwa na mguu wake uliobabuka ngozi kutokana na sumu ya nyoka naye amefariki! Sababu, mguu wake ulivimba tena na kubadilika tena rangi, ukawa mweusi zaidi kisha mwili wote ukavimba na alikata roho ndani ya saa ishirini na nne tu!
Nikahofia kuwa labda na mimi niko kwenye mkumbo huohuo kwa kile kilichoaminika kwa wakazi wa hapo kuwa yule hakuwa nyoka wa kawaida, ni joka la miujiza. Ni jini!
Mtaa huo ukawa ukiogopwa na wakubwa kwa wadogo. Nilithibitisha kuwa mtaa huo ulikuwa ukiogopwa na watu kwa kipindi hicho siku nilipopewa lifti ya gari nikielekea maeneo ya Posta Mpya na kutomwona mtu hata mmoja akitembea barabarani hapo hadi Mwembejini!
Hata akinamama waliokuwa wakipeleka biashara mjini maarufu kwa ‘mamantilie iliwalazimu kukusanyana hadi kufikia kumi au zaidi kisha wanasindikizwa na wanaume wawili au watatu wakiamini kuwa ndiyo salama yao!
Mtaa wa Ngano ukageuka kuitwa kimasihara kwa jina LA ‘Mtaa wa Nyoka!’
Guu langu liliendelea kuwa jeusi japo halikubabuka. Mwezi ukaisha nikiwa siwezi kuvaa kiatu. Mwezi wa pili ukakatika! Lakini nafuu ilizidi kupatikana. Hatimaye siku ya Jumapili ya Pasaka mwezi Aprili, nikafumba macho na kuvaa viatu huku nikijisemea ‘liwalo na liwe’ kama ni kukatwa mguu basi na nikatwe.
Nilifikia hatua ya kuchukua uamuzi huo kwa kuwa kuna daktari mmoja alinihadharisha kuwa nikivaa kiatu wakati bado sumu haijateketea mguuni basi mguu utaoza!
Nilishachoka kupita mitaani na sandozi!
Siku hiyo ya Pasaka nikavaa viatu na kwenda kanisani. Ukawa mwanzo wa kupona. Badala ya maumivu kuongezeka, yakawa yanapungua kila kukicha. Taratibu rangi ya ngozi ikaanza kurudi. Hadi leo niko vizuri na mtaani hapo kuko kawaida. Mtaa unapendeza maradufu!
Hakuna wa kuumwa nyoka wala tandu! Tofauti ni kuwa ile miti iliyopandwa kando ya barabara imekuwa mikubwa zaidi na imestawi zaidi, kiasi cha kutoa taswira ya kuvutia machoni mwa yeyote apendaye mazingira ya aina hiyo.
Kijani kitupu! Mchana kuna kivuli kizito!
Sasa ukipita usiku barabarani hapo giza lake ni zaidi ya giza. Kama una moyo mwepesi, utageuza njia urudi ulikotoka!
*****MWISHO.*****
0 Maoni